Unordered List

Pages

Tuesday, January 1, 2013

MWANAJESHI ALIYEPIGA PICHA NA LEMA ATOROKA

>>> JESHI LAENDELEA KUMSAKA



JESHI la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), limesema askari anayedaiwa kuwa jeshi hilo aliyepiga picha na Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema ametoroka.
Msemaji wa JWTZ, Kanali Kapambala Mgawe alisema jana kwamba pamoja na hatua yake ya kutoroka, jeshi litaendelea kumsaka kwa udi na uvumba ili kumhoji na kujiridhisha kama kweli ni mwanajeshi wake kabla ya kumchukulia hatua za kinidhamu kwa mujibu wa Kifungu cha 147 cha Katiba ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ya 1977.
“Huyu kijana inasemekana alishawahi kupitia Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), lakini wakati tunaendelea na uchunguzi alitoroka katika nyumba aliyokuwa amepanga bila ya taarifa kwa baba mwenye nyumba,” alisema Kanali Mgawe na kuongeza:
“Askari huyo alikuwa anaishi katika nyumba ya kupanga mita chache karibu na Kituo cha Polisi cha Simanjiro, Arusha na alikuwa akijishirikisha na ulinzi shirikishi.”
Alipoulizwa jina la askari huyo, Kanali Mgawe alijibu: “Yeye alikuwa anafahamika mtaani hapo kwa jina la kamanda.”
Hata hivyo, Kanali Mgawe alisema jeshi hilo litahakikisha linatoa ripoti kamili kwa umma baada ya kumkamata na uchunguzi kukamilika ili kuondoa utata uliogubika suala hilo.
Alipoulizwa kama kuna tofauti gani kati ya mwanajeshi kuingia kwenye mikutano ya wanasiasa na wale wanaofanya kazi za kisiasa kama wakuu wa wilaya na mikoa, Kanali Mgawe alijibu:” Wanajeshi wanaofanya kazi za U-DC au RC, wanaruhusiwa kisheria.”
Alifafanua kuwa iwapo mwanajeshi atateuliwa kufanya kazi katika taasisi yeyote ya Serikali nje ya jeshi, atatakiwa kuvua magwanda ya jeshi na kufanya kazi hiyo mpaka atakapomaliza muda wake na baada ya hapo ataruhusiwa kurejea jeshini.
“Kuna kitu kinaitwa ‘secondment.’ Mwanajeshi anaruhusiwa kufanya shughuli zozote nje ya jeshi iwapo atahitajika kufanya hivyo. Ila kwa masharti ya kuvua magwanda, hivyo wananchi wasishangae kuwaona baadhi ya askari wetu ni wakuu wa wilaya na mikoa na baadaye kurudi jeshini kuendelea na majukumu yao,” alisema Kanali Mgawe na kuongeza:
“Askari akiwa katika majukumu yake mapya, atafanya kazi zote atakazopewa zikiwamo za kisiasa kama ilivyo kwa wakuu wa wilaya na mikoa, lakini akirudi jeshini, anarudi kuwa askari mwenye utii na kufuata kanuni za jeshi zisizofungamana na siasa.”

Saturday, December 29, 2012

MNYIKA-TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI



Nakusudia kutumia kifungu cha 10 cha Sheria
ya ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kutaka nakala ya mkataba wa mkopo wa masharti kiasi cha Dola za Marekani bilioni 1.225 (shilingi trilioni 1.86) kutoka China.

Nitataka pia nakala za mikataba wa mradi wa miundombinu ya gesi asilia ambayo itahusisha ujenzi wa mitambo ya kusafishia gesi asilia katika mikoa ya Lindi na Mtwara na ujenzi wa bomba kuu la kusafirishia gesi asilia la inchi 36 kutoka Mtwara kupitia Lindi, Pwani hadi Dar es Salaam lenye umbali wa kilometa 532.

Hii ni kwa sababu mpaka sasa Wizara ya Nishati na Madini haijatekeleza pendekezo nililowasilisha bungeni tarehe 27 Julai 2012 kwamba kutokana na unyeti wa mradi huo kwa mustakabali wa nchi na maisha ya wananchi wa sasa na baadaye Serikali ilipaswa kuwasilisha bungeni na kuweka wazi kwa umma mkataba wa mradi husika.

Pendekezo hilo lingeliwezesha Bunge kuishauri na kuisimamia serikali kuanzia katika hatua za awali kuhakikisha kwamba maslahi ya taifa yanalindwa katika hatua zote na pia wananchi wananufaika kutokana na fursa za uwekezaji huo mkubwa.

Kutokana na Serikali kutokuzingatia pendekezo hilo na badala yake Rais Jakaya Kikwete kufanya uzinduzi wa mradi huo tarehe 8 Novemba 2012 Mkoani Dar es salaam huku usiri ukiendelezwa malalamiko yameanza kujitokeza katika maeneo ya mradi husika hususan katika Mkoa wa Mtwara.

Aidha, Serikali irejee katika mapendekezo niliyotoa bungeni na kutoa maelezo kwa umma ya sababu za bomba hilo kujengwa kutoka Mtwara mpaka Dar es salaam na kueleza kwa uwazi manufaa ya mradi huo na miradi mingine inayopaswa kutekelezwa katika mikoa ya Kusini kwa maendeleo ya wananchi husika.

Tarehe 27 Julai 2012 nilieleza bungeni kuwa pamoja na ujenzi wa mitambo miwili ya kusafishia gesi asili Mnazi Bay na Songo Songo kama sehemu ya mradi huo; Serikali inapaswa kueleza ni miradi ipi inayoambatana na mradi huo ambayo imepangwa kuwanufaisha wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara ikiwemo kuharakisha utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa MW 300 Mtwara na MW 230 wa Somanga Fungu (Kilwa).

Kwa upande mwingine, utekelezaji wa mradi huo unaendelea bila kuwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo ingepaswa kuishauri na kuisimamia Serikali hivyo ni muhimu Spika wa Bunge akachukua hatua kutokana na barua niliyomwandikia mwanzoni mwa mwezi Oktoba 2012 ambayo mpaka sasa haijajibiwa.

Ikumbukwe kwamba katika barua hiyo nilitoa mwito kwa Spika atumie madaraka na mamlaka yake kutangaza kwa umma kamati nyingine ya kudumu ya Bunge itayoshughulikia nishati na madini ikiwemo masuala ya gesi asili kwa sasa kufuatia hali tete na tata kuhusu sekta ndogo ya gesi asilia nchini na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

Pamoja na mambo mengine nilipendekeza Spika aelekeze kamati hiyo kupokea na kujadili Taarifa ya Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge ya mwaka 2011 kuhusu Sekta Ndogo ya Gesi Asili ikiwemo juu ya hatua iliyofikiwa katika kushughulikia tuhuma za ufisadi, madai ya mapunjo ya fedha za mauzo ya Gesi asili na hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya sera, mpango mkakati na sheria ya gesi asili.

Hatua hii ni muhimu kwa sasa kwa kuwa hata baada ya uamuzi wake kuhusu tuhuma za rushwa kwa wajumbe wa Kamati husika, Spika hakueleza hatma ya Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa hali ambayo imeacha ombwe la uongozi na usimamizi wa kibunge (Parliamentary Oversight) kwenye sekta hizi nyeti kwa uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini

Wednesday, November 28, 2012

Wabunge wa Kigoma wamtunishia misuli RC

Wabunge wa Mkoa wa Kigoma wamemtunishia misuli Mkuu wa Mkoa huo, Kanali Mstaafu Issa Machibya, kutokana na kuwatishia kuwafunga pingu kama raia wengine wa kawaida, wakisema kauli hiyo ni dharau kubwa kwao wakiwa ni moja ya mihimili mitatu ya dola wenye jukumu la kuishauri na kuisimamia serikali, hivyo anapaswa kuwaomba radhi.
Kanali Machibya anadaiwa kutoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita mbele ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, katika kongamano la uwekezaji Kanda ya Ziwa Tanganyika, mkoani Katavi, kwa kutamka kwamba, mbunge yeyote atakayekaidi maelekezo yake au maelekezo ya mkuu wa wilaya atakamatwa na kupigwa pingu kama raia wengine wa kawaida.
Wakuu wa mikoa mitatu inayounda ukanda huo, ambayo ni Kigoma, Katavi na Rukwa, walihudhuria kongamano hilo pamoja na wakuu wa wilaya na watendaji wengine, wakiwamo makatibu tawala wa mikoa (RAS)na wilaya (DAS).

MOSES MACHALI
Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali, alisema jana kuwa kwa kauli hiyo, Kanali Machibya ameonyesha kuwadharau wabunge kwamba, ni watu wasiofikiria.
“Kwa hiyo, tunamtaka ombe radhi. Aelewe kwamba, tunafanya kazi zetu kwa mujibu wa sheria. Hivyo, anapaswa aheshimu mhimili wa wabunge,” alisema Machali.
Alisema kauli hiyo ya Machibya ni ya kipuuzi na pia ni ya kifedhuli uliopindukia kwani imeonyesha mkuu huyo wa mkoa ana uwezo mdogo wa kufikiri kinyume cha ulimwengu wa sasa ulivyo.
Machali alisema Machibya anasahau kuwa yeye si bosi wa wabunge na kwa hiyo, hawezi kumfunga mbunge yeyote pingu kama anavyotamba.
Alisema kama itatokea mbunge akampinga mkuu wa mkoa, basi atakuwa ana sababu za msingi za kufanya hivyo.

Thursday, November 22, 2012

SEHEMU YA PILI: Mahojiano ya moja kwa moja na Mhe. Zitto Zuberi Kabwe katika JamiiForums


MHOJAJI: Mkuu Zitto nashukuru kwa majibu yako kina kwa swali la kwanza, swali linalofuata;

B. Zitto na CHADEMA

1) Nini kipaumbele chako cha sasa kama mwanachama wa CHADEMA?

2) Mkuu, ni kweli kuwa CHADEMA ni chama cha kidini/kikabila? Na kama ni kweli, tatizo hilo lishughulikiwe vipi? Kama si kweli, unaweza kuueleza umma wa watanzania una kauli gani juu ya mitizamo hii dhidi ya chama chenu?

3) Mh. Zitto, unaizungumziaje demokrasia ndani ya chama chako katika chaguzi, teuzi na kupanga safu za uongozi?

4) Kwanini CHADEMA haiwatumii viongozi wa Mikoa na Wilaya na badala yake inatuma watu toka makao makuu hata kwa mambo madogo madogo ambayo yangemalizwa na uongozi wa ngazi husika?

5) Mh Zitto, unazizungumziaje harakati za M4C na athari (impact) yake kisiasa na kijamii? Chama kimeweka taratibu gani nzuri za malezi kwa wanachama wapya wanaojiunga kwenye M4C, kama bado, huku si kusuka kamba inayoungua?

6) Inadaiwa hushiriki kikamilifu M4C, ni kweli? Nini kauli yako dhidi ya tuhuma hizi?

7) Je, utaratibu wa kupita mikoani katika kutafuta nafasi ya kugombea uenyekiti kama ilivyokuwa wakati wa Mbowe unafaa au CHADEMA irudi katika utaratibu kama wa CCM?

8) Mhe. Zitto, Viongozi/CHADEMA imekuwa mstari wa mbele kufichua ufisadi. Kuna taarifa kuwa kuna mwanachama wenu katafuna fedha za M4C, ni kweli? Kama ni kweli, ameshughulikiwaje? Kama hajashughulikiwa, ni kwanini mko kimya?

9) Zitto wewe ni naibu katibu mkuu wa CHADEMA, Mara nyingi matamko ya chama yametolewa na Katibu, Mwenyekiti, Mnyika (tangu kabla hajawa msemaji) na mara chache wanasheria km Lissu, Marando na Prof.Safari. Kwanini Zitto umekuwa mbali sana na matamko haya ya CHADEMA ukiwa kama Naibu Katibu mkuu? (Naamini hutojibu ni mgawanyo wa kazi)

10) Unafikiri CHADEMA uliyoikuta mwanzo ndiyo hii ya sasa au kuna mabadiliko? Kama kuna mabadiliko ni yepi na unafanya nini kufanya CHADEMA iwe kama ambavyo ulitaka iwe?

11) Unafikiri namna CHADEMA inavyoendesha siasa zake kuna uwezekano wa kushika dola mapema (2015)? Kama ndiyo kwanini na kama hapana unafikiri mabadiliko gani yanatakiwa kufanyika kuelekea 2015?

12) CCM wanadai kuwa nyinyi CHADEMA hamna presidential materials, una kauli gani juu ya hili?

13) Una muono gani kuhusu upinzani nchini na nini nafasi ya upinzani hasa CHADEMA kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ukilinganisha na chama tawala CCM?

ZITTO: Nitajibu tena kidogo kidogo maana hii peke yake ina maswali 13. 
1.Nini kipaumbele chako cha sasa kama mwanachama wa CHADEMA? 
 
 - Kutumikia chama chetu kwa nafasi nilizonazo.

Natumia nafasi yangu ya Ubunge na Uwaziri kivuli kuhakikisha kuwa chama kinapata taswira chanya mbele ya jamii, Na kinaleta mabadiliko ambayo chama tawala, yaani CCM, kinashindwa kuwafikishia wananchi. Utaona kwamba, kama unafuatilia Bunge, hakuna mkutano wa Bunge unaopita bila hoja mahususi inayojenga taswira chanya ya chama.

Ni bahati mbaya sana kuwa hatutumii baadhi ya mafanikio yetu Bungeni kwenye ulingo wa siasa ma hivyo kuwaacha CCM wanachukua credits.

Kwa mfano, ni kwanini mafanikio ya hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu hatujayafanyia kazi ya kisiasa? Ingawa hatukufanikiwa kumtoa Waziri Mkuu lakini tuliilazimisha Serikali kufanya mabadiliko. Kikwete alisema ni upepo tu, lakini upepo huu ulikuwa na joto kali ukamshinda na tukaacha yeye achukue credit kwa kazi yetu ya uwajibikaji.

Hoja ya juzi ya Mheshimiwa Halima Mdee kuhusu Ardhi inabidi kuifanya ni ajenda ya kisiasa. Hoja ya Mkonge tulikwenda Tanga na ilikuwa na mafanikio makubwa sana. Hoja ya Mabilioni ya Uswiss nayo tunaiachia wanaisemea watu wa CCM kuififiza. Historia inatuonyesha kuwa hoja zote tulizozitumia vizuri nje ya Bunge zilijenga taswira nzuri ya chama ie Buzwagi na EPA. We ignore this at our own peril
 
2.Mkuu, ni kweli kuwa CHADEMA ni chama cha kidini/kikabila? Na kama ni kweli, tatizo hilo lishughulikiwe vipi? Kama si kweli, unaweza kuueleza umma wa watanzania una kauli gani juu ya mitizamo hii dhidi ya chama chenu?
 
- Chadema ni chama cha kitaifa. Kingekuwa chama cha kidini au kikabila kingefutwa. Katika uongozi wa Chadema unapata watu toka mikoa na kabila mbali mbali, pia watu toka dini mbali mbali. Diversity hii haipatikani katika vyama vingi humu nchini. Nadhani mtazamo huu unapandikizwa na watu ambao hawakipendi chama chetu na wanao ona chama kama threat kwa maslahi yao binafsi.

Pia sisi kama chama tunapaswa kuwa makini sana, hasa viongozi tunapofanya kazi zetu ili kutothibitisha taswira hii mbaya dhidi ya chama chetu. Baadhi ya wanachama wa CHADEMA ndio mabingwa wa kueneza jambo hili. CCM nao humo humo wanapandikiza mbegu za chuki. Unakuta Waziri wa CCM anamwita Mbunge wa CHADEMA na kumwambia, fulani bwana mdini sana. Mwangalieni. Kiongozi wa CHADEMA anajiona kapata bonge ya issue na kueneza. Tunachinjwa na CCM kwa upuuzi wetu. Kwa ujinga wetu wenyewe. Chama chetu kimesambaa nchi nzima na viongozi wake ni wa dini zote na makabila yote.

3.Mh. Zitto, unaizungumziaje demokrasia ndani ya chama chako katika chaguzi, teuzi na kupanga safu za uongozi?
 
CHADEMA ina demokrasia ya aina yake na wanachama tunaridhika nayo. The Party deploys for or against your wishes and every member must oblige a just deployment. Tuna utaratibu mzuri sana wa kujieleza na kutetea hoja zetu ndani ya chama, na baada ya watu wote kukubaliana tuna hakukusha tunasimama wote kwa kauli moja sehem zote tunapo wakilisha chama. Sio katika kupanga safu za uongozi tu, ni sehem zote za uongozi wa chama.

4.Kwanini CHADEMA haiwatumii viongozi wa Mikoa na Wilaya na badala yake inatuma watu toka makao makuu hata kwa mambo madogo madogo ambayo yangemalizwa na uongozi wa ngazi husika?
 
Huo mtazamo unaweza kutokana na kulinganisha Chadema na vyama vingine. Ieleweke kua Chadema ni chama tofauti na kina utaratibu wake. Katika chama chetu Viongozi wa mikoa na wa wilaya wana majukumu yao, na makao makuu pia yana majukumu yake.

Inaweza kutokea mara kwa mara hizi level mbili zishirikiane katika kutekeleza kazi za chama. Hata hivo, tunaendelea kujenga chama kama taasisi, hivyo tunaendelea kujenga uwezo wa viongozi wetu wa mikoa na wilaya ili waweze kumudu majukumu mengi zaidi na kuwaachia wenye kukaa makao makuu kuhusika zaidi na strategies za chama.
5.Mh Zitto, unazizungumziaje harakati za M4C na athari (impact) yake kisiasa na kijamii? Chama kimeweka taratibu gani nzuri za malezi kwa wanachama wapya wanaojiunga kwenye M4C, kama bado, huku si kusuka kamba inayoungua?
 
Kwa sababu jina lake liko wazi kabisa, M4C ni moja ya operesheni inayo fanikisha watanzania kujiunga katika chama huku wakijua kabisa kua malengo ni kuleta mabadiliko chanya.

Impact yake kwa jamii ni kubwa sababu inawaweka wanachama wenyewe kua vyanzo vya mabadiliko. Baada ya kujiunga, ni obvious kua Chama kinatoa mafunzo kwa wanachama wake wapya na hivyo kuwalea kuwa makada wazuri. Hii sio opresheni ya kwanza ya Chama, na haitakua ya mwisho.

M4C sio chama ndani ya chama, M4C ni operesheni ya kujenga chama na kuleta mabadiliko nchini.
 
6.Inadaiwa hushiriki kikamilifu M4C, ni kweli? Nini kauli yako dhidi ya tuhuma hizi? 
 
 Ninashiriki sana kazi za kujenga chama. Nimeshiriki sana operesheni mbalimbali za chama. Nitaendelea kushiriki nikiwa mwanachama na kiongozi wa chama.

Halikadhalika wengine tunashughulika zaidi katika kuwakilisha chama Bungeni na mikakati mengine ya kuhimarisha chama, ila tukipata nafasi tunajiunga pia katika kazi za kujenga chama. Mikutano yetu ya chama tunagawana maeneo.

Mimi, kwa mfano kwenye M4C nimepangiwa mkoa wa Manayara na Singida nikiwa na Tundu Lissu na Christina Lissu na Rose Kamili. Mtakumbuka mwanzo mwa mwaka nilifanya ziara Tanga bila viongozi wenzangu. Mtakumbuka nilikwenda Marekani kufungua tawi la chama kule. Nimefanya mikutano Iringa, Hanang nk. Nimeshiriki kampeni za udiwani maeneo mbalimbali nchini. Siwezi kuonekana kila mkoa kila wakati. Pia ninapangiwa kazi.
 
7.Je, utaratibu wa kupita mikoani katika kutafuta nafasi ya kugombea uenyekiti kama ilivyokuwa wakati wa Mbowe unafaa au CHADEMA irudi katika utaratibu kama wa CCM?
 
Hatujawahi kufanya utaratibu unaosema isipokuwa kwenye Urais mwaka 2005. Hatujarejea tena utaratibu huo. Mfumo wowote ambao unapanua demokrasia ya chama ni bora zaidi katika kuimarisha chama. Chama kinakomaa kwa wanachama kushindana kwenye chaguzi za ndani. Natumai uchaguzi mkuu ujao wa chama utakuwa na wagombea wengi zaidi ili wanachama wapate uchaguzi wa kweli. Sipendi chaguzi za kupita bila kupingwa katika chama kinachotaka kujenga demokrasia ya nchi.

8.Mheshimiwa Zitto Viongozi/CHADEMA imekuwa mstari wa mbele kufichua ufisadi. Kuna taarifa kuwa kuna mwanachama wenu katafuna fedha za M4C, ni kweli? Kama ni kweli, ameshughulikiwaje? Kama hajashughulikiwa, ni kwanini mko kimya?
 
Nasikia suala hili hapa, tupeni ushahidi na tutachukua hatua mara moja.

9.Zitto wewe ni naibu katibu mkuu wa CHADEMA, Mara nyingi matamko ya chama yametolewa na Katibu, Mwenyekiti, Mnyika (tangu kabla hajawa msemaji) na mara chache wanasheria km Lissu, Marando na Prof.Safari. Kwanini Zitto umekuwa mbali sana na matamko haya ya CHADEMA ukiwa kama Naibu Katibu mkuu? (Naamini hutojibu ni mgawanyo wa kazi)
 
Naibu Katibu Mkuu sio msemaji wa chama. Katika kujibu suala la demokrasia katika chama nilisema kuwa kuna utaratibu wa kujadili hoja mbali mbali ndani kwa ndani, yakiwemo matamko ya chama.

Katibu mkuu wa CHADEMA anapotoa matamko ya chama anatoa yale yaliyojadiliwa na wanachama wote, nikiwemo mimi, hivyo kuwakilisha maoni yangu pia. Sidhani kama kuna umuhimu wa kuifanya kazi hiyo wakati nimeridhika kua maoni yangu yanawakilishwa kupitia utaratibu wa chama.

10.Unafikiri CHADEMA uliyoikuta mwanzo ndiyo hii ya sasa au kuna mabadiliko? Kama kuna mabadiliko ni yepi na unafanya nini kufanya CHADEMA iwe kama ambavyo ulitaka iwe?
 
CHADEMA ni chama kinachokua kwa kasi sana, na kadiri kinavyokua kinabadilika positively. Moja ya mabadiliko hayo ni idadi ya wanachama, nyingine ni kuweza kushika Uongozi wa Upinzani Bungeni, nafasi ambayo ilikua ya CUF nilipo ingia chama. Chama hivi sasa kipo kila mahala.

Nakumbuka mwaka 2005 tulikwenda Mafinga kuhutubia tukapata watu 20 tu kwenye mkutano. Leo tunaombwa kwenda huko. Chama kina influence maamuzi ya nchi hivi sasa. Hayo yote ni mabadiliko makubwa na mazuri, na ninafurahi kuwa sehemu ya mafanikio ya chama changu.

11.Unafikiri namna CHADEMA inavyoendesha siasa zake kuna uwezekano wa kushika dola mapema (2015)? Kama ndiyo kwanini na kama hapana unafikiri mabadiliko gani yanatakiwa kufanyika kuelekea 2015?
 
Sina mashaka na hili. Nitafafanua zaidi baadaye
 
12.CCM wanadai kuwa nyinyi CHADEMA hamna presidential materials, una kauli gani juu ya hili?
 
Kweli unategemea kuwa chama tawala kinaweza kukisifu chama cha upinzani kwa kuwa na presidential material? Mimi ni Presidential material kwa mfano.

Nina Uwezo, Uadilifu na Uzalendo wa kuweza kuwa Amiri Jeshi Mkuu. Dkt. Slaa ni Presidential Material. Mbowe ni Presidential material. Kitila Mkumbo ni Presidential material. Wapo wengi sana ndani ya CHADEMA wenye sifa za kuwa Marais. Sina mashaka kabisa hilo.

13.Una muono gani kuhusu upinzani nchini na nini nafasi ya upinzani hasa CHADEMA kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ukilinganisha na chama tawala CCM?
 
Ili Tanzania iwe salama ni lazima CCM ishindwe uchaguzi. CCM ikishinda tena mwaka 2015 itavunja sana moyo wa wananchi na wengine wanaweza kukata tama. Lakini pia CCM imechoka na haina nguvu za kutosha kukabiliana na changamoto za nchi hivi sasa.

Njia pekee ya kuisadia CCM iweze kujipanga upya ni yenyewe kondoka madarakani. CHADEMA ina nafasi kubwa sana ya kushinda na kuongoza dola. Muhimu chama kijipange na kuonekana kama chama kilichotayari kushika dola. Tuyatende tunayoyasema na tujiimarishe zaidi.
 
MWISHO WA SEHEMU YA PILI SUBIRI SEHEMU YA TATU

Wednesday, November 21, 2012

KAMA HUKUPATA NAFASI YA KUSOMA MAHOJIANO YA ZITTO KWENYE JAMII FORUM NAKULETEA MAHOJIANO YA AWALI

>>MASWALI NA MAJIBU YA ZITTO KABWE NA JF


 ZITTO:Re: Mahojiano ya moja kwa moja na Mhe. Zitto Zuberi Kabwe katika JamiiForums

Awali ya yote itoe shukrani zangu za dhati kwa kupewa fursa hii adimu ya kuhojiwa na wana JF wenzangu.

Nashukuru pia kwa kuwa ni heshima kubwa sana kwangu maana mimi ni mtu wa pili kufanyiwa mahojiano kama haya baada ya kijana mwenzetu Maxence kama 'founder' wa jukwaa letu. Napenda pia ifahamike kuwa mimi ni mmoja wa wanachama waanzilishi wa jukwaa hili na ninafurahi kuona limekuwa na kwa kweli its a force to reckon with.

Zitto ni Mtanzania aliyezaliwa Kigoma, Kijiji cha Mwandiga. Nimekulia katika kitongoji cha Mwanga, nimekwenda shule ya Msingi Kigoma, Sekondari Kigoma, Kibohehe Moshi, Galanos Tanga na Tosamaganga Iringa. Nimepata Elimu ya Juu Chuo Kikuu cha Zanzibar kwa mwaka mmoja, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara ya Uchumi, Scholarship ya InWent Biashara ya kimataifa na Bucerius School of Law and Business Mineral Economics.

Ninaishi Kijijini Kibingo, Kata ya Mwandiga Wilaya ya Kigoma. Pia Tabata wilaya ya Ilala na Dodoma nyakati za Bunge. Ninaishi na mama yangu mzazi na wadogo zangu.

MHOJAJI:A. Zitto na Ombwe la itikadi miongoni mwa vyama vya siasa


Ni dhahiri CCM na Chadema sera zao ni zile zile katika mazingira ya soko huria, tofauti yao pengine ni ukosefu wa sheria zenye meno kudhibiti mambo Fulani Fulani, au mapungufu katika uwajibikaji, utekelezaji n.k; Kutokana na hili, ni vigumu kutofautisha kwa kina CCM ikulu 2015, hasa ile ambayo itaamka kutoka usingizini, na Chadema ikulu 2015 ambayo itapatikana pengine kutokana na vita dhidi ya ufisadi na pia ukali dhidi ya utekelezaji mbovu wa sera za CCM, usimamizi mbovu wa rasilimali za taifa, na tabia ya viongozi kutowajibika.

Hayana yote matatu hayana itikadi, na iwapo CCM itabadilika, Chadema itakuwa katika wakati mgumu kuendelea kuipa ushindani CCM; Ndio maana unakuta comments za Chadema kuhusu mabadiliko ya uongozi CCM etc ni za kuponda tu kwamba ‘hakuna kitakachobadilika’, kwani nje ya kusema hayo, hakuna hoja nyingine yenye mashiko kwani hoja ya ufisadi itapotea hivi hivi….

1. Unalizungumziaje Ombwe la Itikadi Miongoni mwa Vyama vyetu vya Siasa, ambapo tangia mageuzi ya kisiasa na kiuchumi yaingie nchini, ni vigumu kutofautisha itikadi za vyama vya siasa - kinadharia na kivitendo, hasa ukizingitia ukweli kwamba kwa kila chama, sera na itikadi zinazouzwa au kutekelezwa ni za kiliberali, huku wananchi wengi (hasa vijijini) wakiwa hawana ufahamu juu ya madhara na faida ya itikadi hii ni nini.

2. Unaiongeleaje sera ya Majimbo ya CHADEMA?

3. Unaona tofauti ya msingi kati ya CCM na CHADEMA ni IPI?

4. Nini kinakuvutia ndani ya CCM ambacho hakipo CHADEMA?

5. Bado unafikiri wewe kuwa CHADEMA ni tija kwa jamii kuliko kuwa Chama kingine mfano CCM?

6. Unalizungumziaje suala la kuwa na utitiri wa vyama vingi vya siasa vinavyokula pesa za walipa kodi halafu havina tija wala mchango wowote kijamii zaidi ya kutufilisi, je kuna umuhimu wa kuifanyia sheria mabadiliko ili kuwe na limitation mfano, vyama vitatu tu?


ZITTO:

Maswali marefu sana. Nitajibu kidogo kidogo.

1. Unalizungumziaje Ombwe la Itikadi Miongoni mwa Vyama vyetu vya Siasa, ambapo tangia mageuzi ya kisiasa na kiuchumi yaingie nchini, ni vigumu kutofautisha itikadi za vyama vya siasa - kinadharia na kivitendo, hasa ukizingitia ukweli kwamba kwa kila chama, sera na itikadi zinazouzwa au kutekelezwa ni za kiliberali, huku wananchi wengi (hasa vijijini) wakiwa hawana ufahamu juu ya madhara na faida ya itikadi hii ni nini.

- Hii ni changamoto kubwa sana kwa nchi yetu. Itikadi za kisiasa husaidia kunyoosha sera za vyama. Hivi sasa chama chochote chaweza kuwa na sera yeyote ile kwa kuwa hakuna uti wa mgongo ambao ni itikadi. Lazima vyama vijipambanue kwa itikadi zao. Kwa kukosekana kwa itikadi zinazoeleweka vyama vimekuwa kama 'electoral machines' tu. Kukosekana kwa itikadi kunafanya vyama kudandia masuala. Mfano juzi hapa mmesikia Mkutano Mkuu wa CCM umeazimia elimu iwe bure.

CHADEMA tulisema hivi mwaka 2010, CCM wakasema huo ni uwendawazimu kwani haiwezekani. Nakumbuka nilikuwa kwenye mdahalo pale Serena (hivi sasa) mwaka 2010, vijana wa CCM wakaniuliza mtapata wapi pesa za kusomesha watu bure. Nikawajibu kama tuliweza kuwasomesha bure kwa Tumbaku, Kahawa na Pamba, tutawasomesha bure kwa dhahabu, tanzanite nk. Leo CCM wanasema elimu bure. Nimemsikia Lowassa juzi anasema inawezekana. Lowassa huyu nilibishana naye sana mwaka 2010 akisema haiwezekani. Huu ni ukosefu wa itikadi sahihi.

Sababu kubwa pia viongozi wetu hawasomi na hivyo bongo zao hazipo 'sharp' kuweza kuona ni mwelekeo gani wa itikadi wa kufuata. At best tunaimba kama kasuku itikadi zilizoendelezwa nje, hakuna originality
2.Unaiongeleaje sera ya Majimbo ya CHADEMA? 
 - Ni utekelezaji wa kushusha madaraka mikoani, kupanua uwajibikaji na kuleta maendeleo kwa wananchi. Sera hii ya utawala ndio suluhisho la masuala mengi ya uwajibikaji hapa nchini. Kuna haja ya kuwa na DC? Kwa nini wakuu wa mikoa wasichaguliwe na wananchi? Tulipoamua kupendekeza sera hii kwa wananchi kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 tuliambiwa sisi tuna lengo la kuleta ukabila nchini. Inawezekana kuna maeneo fulani fulani tulikosea mkakati. Kwa mfano tulianza kusemea suala hili tukiwa mkoani Kilimanjaro, kwa hiyo CCM ikadakia 'unaona wachaga hawa' sasa wanataka ka nchi kao. Kimkakati tulikosea.

Tulipaswa kuzindua sera hii kanda ya Ziwa au kanda ya Kusini. Tulijifunza kutokana na makosa haya. Hivi tumejiandaa vizuri zaidi kuielezea sera hii. Tunataka kuimarisha Halmashauri za Wilaya/Miji/Manispaa/Majiji kwa kuoondoa nafasi ya Wakuu wa Wilaya na kada nzima pale Wilayani. Majukumu yote ya kisiasa ya DC atayafanya Mwenyekiti wa Halmashauri. Majukumu yote ya Kiutendaji ya Ofisi ya DC atayafanya Mkurugenzi wa Halmashauri. Wakuu wa mikoa wachaguliwe na Wananchi moja kwa moja na wawe na 'executive powers' kwa mambo ya mkoa husika. Tutayaweka kisheria mambo haya. Hii mambo ya Rais kuteua wakuu wa Mikoa nchi nzima hapana. Watu wachaguliwe.

Ninaamini kabisa kuwa Sera hii ikitekelezwa tutaweza kutumia rasilimali zetu vizuri na mikoa itashindana kimaendeleo badala ya kushindana kwa namna walivyompokea Rais mkoani kwao

MAHOJIANO YA ZITTO KABWE LIVE MUDA HUU JAMII FORUM


Mahojiano ya moja kwa moja yameanza katika thread hii - Mahojiano ya moja kwa moja na Mhe. Zitto Zuberi Kabwe katika JamiiForums

Na hivyo mnakaribishwa kufuatilia, thread hii ni kwa ajili ya side comments na ile ya mahojiano itaendeshwa na AshaDii na atakuwa anajibizana na Mhe. Zitto.



FUATILIA MAHOJIANO HAYO HAPA KWA KUBONYEZA LINK HII>>>>>>>>>>>>>>>>>>
 

Monday, November 19, 2012

J.K ni Jembe. ## MAKALA FUPI KUTOKA KWA MJENGA WA "JF"


Haina ubishi kuwa J. Kikwete ni rais pekee ametawala kwa mizengwe lakini namna anavyoipangua mizengwe hiyo, anastahili pongezi kubwa. Ikumbukwe zengwe la kwanza ni lile la kukataliwa na CHADEMA kuwa si rais halali, wakaenda mbali zaidi kwa wabunge wake kumzilia hotuba yake ya ufunguzi na kutoka nje ili kumdhalilisha, huku katibu mkuu kutangaza kuwa atahakikisha J.K hatawali.

Kikwete kwa umahiri mkubwa alitulia na kuendelea kuhutubia huku akiwahakikishia kuwa "ipo siku watarudi kwake" (walirudi hawakurudi?). Zengwe lingine ni la kudai kumshtaki J.K kwa wananchi ili kumshinikiza aondoke madarakani. Hili pia lilifanywa na CHADEMA kupitia maandamano sehemu mbalimbali za nchi wakilenga zaidi kutengeneza propaganda ya kuidanganya jumuiya ya kimataifa kuwa J.K hakubaliki na wananchi.

Hilo lilishindwa kwakuwa J.K alitulia na wala hakutaka kutumia nguvu ya dola ambao kimsingi ndiyo mtego ulikuwa umewekwa na CHADEMA. Maandamano yaliposhindwa, ukaanza ushawishi wa migomo kwa wafanyakazi walimu na madaktari, nalo lilishughulikiwa kwa umakini kila mtu anajua. Propaganda ya Ulimboka iliyoshikiwa bango na CHADEMA na wanaharakati kwa kumlazimisha Ulimboka aseme hata yasiyokuwepo, iligonga mwamba.

Zengwe zimezidi kuendelea kupitia M4C ya CHADEMA ambayo kwa mgongo wa elimu ya uraia ililenga kushawishi wananchi kuikataa serikali ya J.K kwa mtindo wa Libya, Tunisia na Misri, hiyo nayo nia wazi wananchi wameishtukia kuwa haina nia nzuri na hatma ya Amani ya Tanzania. Imekataliwa na ushahidi ni matokeo ya udiwani wa kata 29 uliofanyika hivi majuzi ambapo CHADEMA pamoja na nguvu kubwa ya M4C iliambulia kata 5! huku CCM ikijikombea kata 22 kati ya 29 zilizokuwa zinagombewa.

J.K amezidi kuimarisha CCM huku CHADEMA wakichelewa kugombania nani agombee urais/uenyekiti wa chama na kibaya zaidi na bila kujijua wote wamejikuta wanaimba wimbo wa CCM na kukiacha chama kikizidi kuangamia. Aliyozuiliwa Zitto kuyafanya, ndiyo yafanywayo na Mbowe.

Juzi juzi hivi Mbowe amesikika akiupongeza urais wa J.K na kukiri kuwa ni urais uliotukuka uliojaa busara na hekima na kwamba kwa TZ hakuna kama J.K. Kimsingi Slaa amejikuta akibaki peke yake aking'ang'ana na siasa za chuki na utovu wa nidhamu kwa J.K huku wenzake wote waliomzunguka wakimuasi bila yeye kujijua. J.K hajateteleka kiutendaji , zaidi ameendelea kukomaa na kujawa na maarifa zaidi.

Sote tumeshuhudia jinsi serikali ya awamu ya nne ilivyovunja rekodi kwa ujenzi wa miundo kupitia hotuba ya Magufuli wakati wa Mkutano mkuu wa CCM Dodoma.

Kwa hakika J.K ni rais ambaye amewabaini wabaya wake mapema na sasa anacheza nao kama atakavyo. Anajua pia wabaya hao bado wanamtafuta kwani bado hawajakidhi haja ya kiu yao ya kuona J.K akitolewa ikulu kwa madai ya kuushindwa Urais. J.K kweli ni zaidi ya "jembe".

SOURCE: JF

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More

 
Powered by Blogger